Thursday, November 6, 2014

Wadau mbalimbali wampongeza Kamishna Jenerali wa Magereza kwa kufanikisha kuandaa rasimu ya sera ya Taifa ya Magereza

 Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, John Casmir Minja akitoa maelezo mafupi katika ufunguzi wa  Mkutano wa kupokea maoni ya Wadau kuhusu Sera ya Taifa ya Jeshi la Magereza ulioanza leo Novemba 04, 2014 katika Hoteli ya Livingstone - Bagamoyo.

Na Lucas Mboje; Bagamoyo

Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, John Casmir Minja amepongezwa na Wadau mbalimbali nchini kwa kufanikisha kuandaa na kukamilisha rasimu ya Sera ya Taifa ya Magereza ambapo Wadau kutoka nje ya Jeshi la Magereza wamepata fursa ya kujadili kwa siku mbili Wilayani Bagamoyo, Mkoani Pwani.

Pongezi hizo wamezitoa kwa nyakati tofauti mjini Bagamoyo katika Mkutano wa siku mbili wa Wadau wa kupokea maoni juu ya rasimu ya Sera ya Taifa ya Magereza uliofunguliwa rasmi na Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Bw.  Mbarak Abdulawakil Novemba 04, 2014 katika Hoteli ya Livingstone - Bagamoyo.

"Tunampongeza sana Kamishna Jenerali Minja hususani kwa kufanikisha rasimu hiyo na tunaamini kutokana na kasi yake ya Utendaji wa kazi rasimu hiyo itawasilishwa mapema Serikali kwa hatua za mwisho," Walisikika wakisema.

Aidha, wameongeza kuwa kukamilika kwa Sera ya Taifa ya Magereza kutaleta ufanisi katika utendaji na uboreshaji huduma mbalimbali zitolewazo ndani ya Jeshi la hilo.

Awali akitoa maelezo mafupi katika ufunguzi wa Mkutano huo wa Wadau wa kupokea maoni ya Sera ya Taifa ya Magereza, Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza nchini, John Casmir Minja alisema kuwa chimbuko la kuwa na Sera hiyo ni kubadili utaratibu wa kuwafunga wahalifu magerezani ambao ulianza wakati wa Ukoloni na ulilenga zaidi kuwakomoa na kuwaadabisha.

Jenerali Minja aliongeza kuwa utaratibu huo ulilenga kuwaweka wahalifu kwenye Ulinzi mkali na kuwafanyisha kazi ngumu zisizo na tija nazisizozingatia haki za Binadamu.

Alisema kuwa baada ya Uhuru mwaka 1961, Falsafa ya Magereza ilibadilika  kutoka ile ya kukomoa na kuwaadabisha wahalifu na kuwa Urekebishaji na kuzingatia haki za Binadamu.

"Mabadiliko ya kifalsafa pamoja na kuridhiwa kwa Mikataba mbalimbali ya Kimataifa yanatulazimu kuwa na Sera ambayo ndiyo itakuwa dira ya Utekelezaji wa shughuli za kila siku za Jeshi la Magereza," alisema Jenerali Minja.

Aidha Jenerali Minja, aliongeza kuwa sera hiyo inalenga pia kubadili mitizamo ya jamii kuwa magereza ni mahali pa mateso. "Tunataka Magereza ya sasa ionekane ni chuo cha kubadili tabia za wafungwa ili wamalizapo vifungo vyao wawe ni raia wema katika jamii."

Jeshi la Magereza kupitia Wataalam wake limeandaa Rasimu ya Sera ya Taifa ya Magereza kwa kushirikiana na Mshauri Mwelekezi toka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Haji Semboja ambapo tayari wadau wote wa ndani na nje ya Jeshi la Magereza wamepata fursa ya kuchangia maoni yao kikamilifu tayari kuwasilishwa rasmi Serikalini kwa hatua za mwisho.