Friday, August 7, 2015

Mazishi ya SACP Aneth Laurent Balibusha

 Marehemu Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza (SACP) Aneth Laurent Balibusha
 Kamishna Jenerali wa Magereza John Minja (wa kwanza kulia), Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mh. Ally Lufunga (wa pili) na Kamishna wa Fedha na Utawala wa Jeshi la Magereza, Gaston Sanga (wa tatu kulia) wakibadilisha mawazo nyumbani kwa marehemu eneo la Segerea, Dar es salaam.
 Mwili wa Marehemu Kamanda Aneth ukibebwa kuingizwa  kwenye gari maalum kwa ajili ya kupelekwa Kanisani
 Mwili wa Marehemu SACP Aneth ukiwasili katika viwanja vya  Kanisa Katoliki Jimbo la Segerea kwa ajili ya kuombewa kabla ya kupelekwa Makaburini.
 Makamanda wakiusindikiza Mwili wa Marehemu Altareni kwa ajili ya kuombewa.
 Baadhi ya Wanafamilia, Ndugu, Jamaa na Marafiki wa Marehemu Kamanda Aneth wakiwa Kanisani wakifuatilia Misa Takatifu.
 Viongozi mbalimbali wa Kitaifa wakiongozwa na Kamishna Jenerali wa Magereza John Minja (wa kwanza kulia)  Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mh.Ally Rufunga (aliyevaa miwani) na aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini Eliakhim Maswi (wa tatu kulia) wakifuatilia Misa ya kumuombea Marehemu Kamanda Aneth Balibusha.
 Sehemu ya viongozi mbalimbali wa Jeshi la Magereza wakifuatilia Misa Takatifu ya kumuombea Marehemu Kamanda Aneth.
Viongozi Waandamizi wa Jeshi la Magereza wakiwa katika ibada maalum ya kumuombea Marehemu. Kutoka kulia ni Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza Dkt. Juma Malewa, Kamishna wa Fedha na Utawala Gaston Sanga, RPO-Mwanza ACP Gorea, RPO-Morogoro SACP Dkt.Katto na RPO-Arusha SACP Nkubasi 
 Paroko Msaidizi wa Parokia ya Segerea Padre Josephat Mmbaga akiubariki mwili wa marehemu Kamanda Aneth Balibusha.
 Paroko Msaidizi wa Parokia ya Segerea Padre Josephat Mmbaga akinyunyuzia maji ya Baraka Mwili wa Marehemu.
Naibu Kamishna wa Magereza Edith Malya akitoa salamu za Jeshi la Magereza kwa niaba ya Kamishna Jenerali wa Magereza kwa ndugu na jamaa waliohudhuria Misa Takatifu kanisani hapo.
 Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mh. Ally Rufunga akitoa salamu kwa niamba ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Shinyanga.
Mwakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi akitoa salamu za Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa niamba ya  Katibu Mkuu wa Wizara hiyo.
Mrakibu Mwandamizi wa Jeshi la Magereza Kasim Mkodo  kutoka Shinyanga akitoa salamu kwa niaba wa watumishi wa Magereza Mkoani Shinyanga.
 Naibu Kamishna wa Polisi DCP Nyamuhanga akitoa salamu za Jeshi la Polisi.
 Kamishna Mstaafu wa Huduma za Urekebishaji wa Magereza  Mama Aziza Sally akitoa salamu kwa niamba ya  Wastaafu wa Jeshi la Magereza lakini pia akiwa mtu aliyefanya kazi kwa muda mrefu na marehemu.
 Kamishna Mkuu Mstaafu, Afande Nicas Banzi akitoa heshima zake za mwisho kwa Mwili wa Marehemu.
 Kamishna Jenerali Mstaafu, Afande Augustino Nanyaro akitoa salamu zake za mwisho kwa mwili wa marehemu.
Waandamizi wa Jeshi la Magereza wakiongozwa na Kamishna Dkt Juma Malewa, Naibu Kamishna Edna Malya,  Kamishna Sanga na Kamishna Msaidizi Mwandamizi Mhandisi Kaluvya  wakipita mbele ya Jeneza kutoa heshima zao za mwisho.


 Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama  aliye pia  Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mh. Ally Rufunga, Kamishna Jenerali John Minja na Eliakhim Maswi wakitoa heshima zao za Mwisho.
 Mfanyakazi wa Jeshi la Mgereza, Ndugu Magret Achwari akilia kwa uchungu wakati wa kuaga mwili wa Marehemu.
 Binti ya Marehemu Kamanda Aneth Bulisha akilia kwa majonzi makubwa wakati wa kumuaga mama yake.
 Baada ya Misa  takatifu ya kumuombea marehemu Msafara wa ndugu jamaa na marafiki ukielekea Makaburini.
 Mwili wa Marehemu Kamanda Aneth ukiwasili  Makaburi ya Segerea tayari kwa mazishi.
 Mwili wa Marehemu SACP  Aneth ukishushwa kaburini
 Paroko Msaidizi wa kanisa Katoliki Jimbo la Segerea Padri Josephat Mmbaga akibariki Kaburi la Marehemu Kamanda  Aneth baada ya mwili kuingizwa kaburini.
 Watoto  wa Marehemu Aneth wakiweka udongo kwenye kaburi kama ishara ya kumuaga mama yao.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mh. Mbaraka Abdulwakil akiweka udongo kaburini.
 Kamishna Jenerali wa Magereza, John Minja akiweka udongo kwenye kaburi.
   Wajukuu wa marehemu wakiweka mashada ya maua kwenye kaburi
 Katibu wa mambo ya Ndani ya Nchi, Mh. Mbaraka Abdulwakil akiweka shada la maua kwenye kaburi.

Kamishna Jenerali wa Magereza John Minja akiweka shada la maua kwenye kaburi.
 Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mh. Ally Rufunga akiweka shada la maua kwenye kaburi.
 Mkuu wa Kikosi cha  Zimamoto Mkoa wa Shinyanga akiweka shada la maua kwenye kaburi.
 Kaburi la Marehemu Kamanda Aneth Bulisha likiwa limepambwa kwa mashada ya maua yaliyowekwa na ndugu, jamaa na marafiki.

Picha zifuatazo ni Gadi maalum ya Mazishi ya Jeshi la Magereza ikitoa heshima za mwisho mbele ya Kaburi la Marehemu Kamanda Aneth Balibusha.





Na ASP Deodatus Kazinja-Makao Makuu ya Magereza
Aliyekuwa Mkuu wa Magereza Mkoa wa Shinyanga Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza (SACP) Anneth Balibusha Laurent umeagwa katika Kanisa Katoliki Parokia ya Segerea  na kuzikwa katika makaburi ya Segerea Jijini Dar es Salaam jana tarehe 06 Agosti, 2015.

SACP Anneth aliugua ghafla tarehe 29 Julai, 2015  Mkoani Shinyanga na kulazwa katika hospatali ya Mkoa huo lakini hali yake iliendelea kubadilika hivyo ikawalazimu kupelekwa katika hospitali ya Rufaa Bungando Mkoani Mwanza kwa matibabu zaidi ambapo jioni ya tarehe 30 Julai, 2015 alifariki dunia.

Akitoa salaam za Jeshi la Magereza katika msiba huo,  Naibu Kamishna wa Magereza (DCP) Edith Malya kwa niamba ya Kamishna Jenerali wa Magereza alisema Jeshi la Magereza na Taifa kwa ujumla limempoteza mtu muhimu aliyekuwa na sifa za pekee katika utendaji kazi wake lakini pia limempoteza katika umri wake mdogo.

Alitoa pole kwa familia, watumishi wa Jeshi la Magereza, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Shinyanga na kwa wote walioguswa na msiba huo. Pia aliitolea mwito familia ya marehemu kuwa wavumilifu katika kipindi hiki kigumu lakini pia kuwa Ofisi yake itaendelea kushirikiana na familia hiyo kwa hali zote.

Aidha alisema kuwa Marehemu Anneth alikuwa miongoni mwa wanawake wachache wenye wadhifa wa Ukuu wa Magereza wa Mikoa hapa nchini ambapo jumla yao wako walikuwa wane tu na hivi sasa wamebaki watatu.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga aliye pia Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Uslama wa Mkoa huo  Ally Nassro Lufunga alisema Kamati yake imempoteza mtu muhimu sana kwani alikuwa ni kiungo katika shughuli zao mkoani lakini pia marehemu alikuwa ameleta mwamko mpya katika vikundi vya akina mama na akiwa kiongozi wa vikundi vya mazoezi nyakati za jioni baada ya kazi. RC Lufunga aliongozana na Kamati yake ya Ulinzi na Usalama katika kumzika mjumbe mwenzao.

Kwa upande wake mwakilishi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa niaba ya Katibu Mkuu alisema Wizara imempoteza mtendaji makini, kwamba wao kama wizara walimtazama Marehemu Aneth kwa kuzingatia umri, elimu , jinsia yake na cheo alichokuwa nacho kama mtu ambaye angekuja kusaidia huko mbeleni katika ule mpango wa kurithishana madaraka. “sisi kiutumishi pale wizarani ni pigo kubwa hatuna jinsi ni mipango ya Mungu  itatubidi kujipanga upya, pole nyote” Alihitimisha

Marehemu Anneth Balibusha Laurent alizaliwa mwaka 1965 katika Kijiji cha Kibwera kata ya Kihanga Wilayani Karagwe Mkoani Kagera. Marehemu  alijunga na Jeshi la Magereza  tarehe 01 Septemba, 1994 akiwa ni Mhitimu wa  Shahada ya Kwanza ya Sanaa katika Uchumi na Mipango  katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM)

SACP Anneth tangu kuajiriwa kwake amekuwa Afisa Mipango Makao Makuu ya Magereza hadi Octoba 2013 alipoteuliwa kuwa Mkuu wa Magereza Mkoani Shinyanga.